الأنفال
Al-Anfal
The Spoils of War
1 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 001
يَسۡـَٔلُونَكَ عَنِ ٱلۡأَنفَالِۖ قُلِ ٱلۡأَنفَالُ لِلَّهِ وَٱلرَّسُولِۖ فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ وَأَصۡلِحُواْ ذَاتَ بَيۡنِكُمۡۖ وَأَطِيعُواْ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥٓ إِن كُنتُم مُّؤۡمِنِينَ
Wanakuuliza juu ya Ngawira. Sema: Ngawira ni ya Mwenyezi Mungu na Mtume. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na suluhisheni mambo baina yenu, na mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake ikiwa nyinyi ni Waumini.
Nabii Muhammad (s.a.w.) katolewa Makka na kalazimishwa kuihama kwa sababu ya vitimbi vya mapagani, washirikina, na kwa kuazimia kwao kumuuwa, ili Waislamu wapate kuwa na dola yao. Naye akenda kukaa Madina kwenye amani na manusura. Huko ikawa hapana budi ila kuwania kujilinda na uvamizi wa maadui, wasije wenye Imani wakapata mateso. Vikatokea hivyo Vita vya Badri. Waumini wakapata ushindi ulio wazi na ngawira nyingi waliziteka. Ikatokea khitilafu kidogo na suala katika shauri la ugawaji wa hizo ngawira. Ndio hivyo Mwenyezi Mungu anasema: Wanakuuliza khabari ya ngawira, zende wapi? Apewe nani? Ni za nani? Zigawanywe vipi? Ewe Nabii! Waambie: Hizo ngawira ni za Mwenyezi Mungu kwanza. Na Mtume, kwa amri ya Mola wake Mlezi, ndiye mwenye madaraka ya kuzigawa. Basi wacheni kukhitalifiana kwa ajili ya hayo. Na uwe mtindo wenu ni kumkhofu Mwenyezi Mungu na kumt'ii. Na tengenezeni yaliyo baina yenu, na mfanye mapenzi na uadilifu ndio makhusiano baina yenu. Kwani hakika hizi ndizo sifa za watu wa Imani.
2 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 002
إِنَّمَا ٱلۡمُؤۡمِنُونَ ٱلَّذِينَ إِذَا ذُكِرَ ٱللَّهُ وَجِلَتۡ قُلُوبُهُمۡ وَإِذَا تُلِيَتۡ عَلَيۡهِمۡ ءَايَٰتُهُۥ زَادَتۡهُمۡ إِيمَٰنٗا وَعَلَىٰ رَبِّهِمۡ يَتَوَكَّلُونَ
Hakika Waumini ni wale ambao anapo tajwa Mwenyezi Mungu nyoyo zao hujaa khofu, na wanapo somewa Aya zake huwazidisha Imani, na wakamtegemea Mola wao Mlezi.
Ama hakika Waumini wa haki na kweli daima wanakuwa na khofu na ut'iifu kwa Mwenyezi Mungu. Akitajwa Allah Subhanahu, Mwenyezi Mungu Aliye takasika, nyoyo zao hufazaika, na zikajaa khofu. Kwa hivyo kila wakisomewa Aya za Qur'ani Imani yao inazidi kuwa imara, na wao huzidi unyenyekevu na ujuzi, na wala hawamtegemei yeyote ila Mwenyezi Mungu aliye waumba, na ndiye anaye walinda na kuwaendeleza.
3 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 003
ٱلَّذِينَ يُقِيمُونَ ٱلصَّلَوٰةَ وَمِمَّا رَزَقۡنَٰهُمۡ يُنفِقُونَ
Hao ambao wanashika Swala na wanatoa katika yale tunayo waruzuku.
Na hao Waumini walio wa kweli katika Imani, wanashika Swala kwa kutimiza nguzo zake, na kukamilisha unyenyekevu na ut'iifu, ili wawe daima katika kumkumbuka Mwenyezi Mungu, na wanatoa katika mali aliyo waruzuku Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taa'la, kwa ajili ya Jihadi, na mambo yote ya kheri, na kuwasaidia wanyonge.
4 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 004
أُوْلَـٰٓئِكَ هُمُ ٱلۡمُؤۡمِنُونَ حَقّٗاۚ لَّهُمۡ دَرَجَٰتٌ عِندَ رَبِّهِمۡ وَمَغۡفِرَةٞ وَرِزۡقٞ كَرِيمٞ
Hao kweli ndio Waumini. Wao wana vyeo, na maghfira, na riziki bora, kwa Mola wao Mlezi.
Hakika hawa wanao sifika kwa sifa hizi ndio khasa wanao sifika kwa Imani kwa haki na kweli. Na malipo yao ni kupata vyeo vya ngazi ya juu kwa Mwenyezi Mungu. Yeye Allah Subhanahu ndiye ataye wapa radhi zake, na maghafira wanapo teleza, na duniani atawapa riziki njema, na Akhera neema ya daima.
5 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 005
كَمَآ أَخۡرَجَكَ رَبُّكَ مِنۢ بَيۡتِكَ بِٱلۡحَقِّ وَإِنَّ فَرِيقٗا مِّنَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ لَكَٰرِهُونَ
Kama Mola wako Mlezi alivyo kutoa nyumbani kwako kwa Haki, na hakika kundi moja la Waumini linachukia.
Ushindi, bila ya shaka, upo mikononi mwa Mwenyezi Mungu. Na funguo za mambo yote ziko kwake. Na hali ya Waumini katika kukhitalifiana kwao katika mambo ya ngawira ni kama hali yao pale alipo kuamrisha Mwenyezi Mungu utoke ukapigane na washirikina katika Badri, nayo ni Haki iliyo thibiti. Kwani miongoni mwa Waumini kulikuwapo na kikundi kilicho chukia vita kweli kweli.
6 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 006
يُجَٰدِلُونَكَ فِي ٱلۡحَقِّ بَعۡدَ مَا تَبَيَّنَ كَأَنَّمَا يُسَاقُونَ إِلَى ٱلۡمَوۡتِ وَهُمۡ يَنظُرُونَ
Wanajadiliana nawe kwa jambo la Haki baada ya kwisha bainika, kama kwamba wanasukumwa kwenye mauti nao wanaona.
Wanajadiliana nawe hao wa kikundi hicho, na wanajaribu kutilia nguvu kauli yao katika jambo la haki, nalo ni kutoka kwa ajili ya Jihadi. Na kumbe wao walikuwa na wenzao walio toka kwenda kupokonya mali ya Makureshi yaliyo kuwa yanakwenda Sham, na wasiyapate. Kikundi hichi kikakhiari kurejea baada ya kuona wamenusurika, kwa kujuvywa na Mtume, na kwamba makafiri wanawaogopa, na kwa kuwa hadi wakivichukia vita, na kuwa hawajui litalo wapata. Na walipo kuwa wakiviendea vita walikuwa kama wanao sukumwa kwenda kufa, na wao wanaona kitacho wauwa, na yanawapata mateso yake.
7 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 007
وَإِذۡ يَعِدُكُمُ ٱللَّهُ إِحۡدَى ٱلطَّآئِفَتَيۡنِ أَنَّهَا لَكُمۡ وَتَوَدُّونَ أَنَّ غَيۡرَ ذَاتِ ٱلشَّوۡكَةِ تَكُونُ لَكُمۡ وَيُرِيدُ ٱللَّهُ أَن يُحِقَّ ٱلۡحَقَّ بِكَلِمَٰتِهِۦ وَيَقۡطَعَ دَابِرَ ٱلۡكَٰفِرِينَ
Na Mwenyezi Mungu alipo kuahidini kuwa moja katika makundi mawili ni lenu. Nanyi mkapenda lisilo na nguvu ndio liwe lenu; na Mwenyezi Mungu anapenda ahakikishe Haki kwa maneno yake, na aikate mizizi ya makafiri.
Enyi Waumini! Kumbukeni ahadi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kwenu kwamba atakupeni ushindi juu ya moja katika makundi mawili, hilo lenye silaha na nguvu. Na hali nyinyi mnapendelea kupambana na hilo kundi jengine lenye mali na watu tu. Na hilo ni msafara wa Abu Sufyan. Nanyi mkakhiari mali yasiyo kuwa na wapiganaji. Lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu anataka kuithibitisha Haki kwa mapendo yake na uwezo wake na kwa maneno yake yaliyo kwisha tangazwa, na ili aung'oe kabisa ukafiri katika Bara Arabu kwa ushindi wa Waumini. Aya hizi tukufu zinatoa sura ya yanayo pita katika nafsi wakati wa vita, nako ni kutamani kukutana na maadui wachache na kuchukia kukutana na wengi, na kupenda kuteka mali na ngawira; na ilhali Mwenyezi Mungu Mtukufu anataka kuitukuza Dini na ishinde Haki na wang'oke makafiri.
8 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 008
لِيُحِقَّ ٱلۡحَقَّ وَيُبۡطِلَ ٱلۡبَٰطِلَ وَلَوۡ كَرِهَ ٱلۡمُجۡرِمُونَ
Ili ahakikishe Haki na auvunje upotovu na wangachukia wakosefu.
Ili athibitishe Haki, na auondoe upotovu, hata wakichukia makafiri ambao wamedhulumu Haki ya Mwenyezi Mungu na Haki ya Waumini na Haki ya nafsi zao wenyewe.
9 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 009
إِذۡ تَسۡتَغِيثُونَ رَبَّكُمۡ فَٱسۡتَجَابَ لَكُمۡ أَنِّي مُمِدُّكُم بِأَلۡفٖ مِّنَ ٱلۡمَلَـٰٓئِكَةِ مُرۡدِفِينَ
Mlipo kuwa mkimuomba msaada Mola wenu Mlezi, naye akakujibuni kuwa: Kwa yakini Mimi nitakusaidieni kwa Malaika elfu wanao fuatana mfululizo.
Na enyi Waumini! Kumbukeni nanyi mnagawana ngawira na mnakhitalifiana, mlipo omba uwokovu na msaada, na mkaandikiwa kuwa hapana la kukuepusheni na vita. Mwenyezi Mungu alikuitikieni maombi yenu, akakuungeni mkono kwa kukuleteeni (Malaika) Roho zilizo safi nyingi zinazo fika elfu zinazo fuatana, zikija moja baada ya moja. Walipo jua wapiganaji Waumini kuwa hapana njia ya kuepukana na vita wakaomba msaada kwa Mwenyezi Mungu, naye Mwenyezi Mungu Mtukufu akawaitikia, na akawaunga mkono kwa Malaika elfu walio fuatana. Yaani alianza kwa kupeleka msaada kwa vikosi vilivyo fuatana ili iwe wepesi kwa kila kikosi kuelekea pahala pake katika vita pasiwepo kukaa bure au kupigana makumbo. Na ifikapo misaada ya majeshi ya vita roho hufurahi na moyo huingia nguvu. Na hayo ndiyo aliyo yakusudia Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kauli yake: "Na Mwenyezi Mungu hakufanya haya ila kuwa ni bishara na ili nyoyo zenu zituwe." Na ushindi daima unatokana na Mwenyezi Mungu.
10 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 010
وَمَا جَعَلَهُ ٱللَّهُ إِلَّا بُشۡرَىٰ وَلِتَطۡمَئِنَّ بِهِۦ قُلُوبُكُمۡۚ وَمَا ٱلنَّصۡرُ إِلَّا مِنۡ عِندِ ٱللَّهِۚ إِنَّ ٱللَّهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ
Na Mwenyezi Mungu hakufanya haya ila kuwa ni bishara na ili nyoyo zenu zituwe. Na haupatikani ushindi ila kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, na Mwenye hikima.
Wala Mwenyezi Mungu Mtukufu hakujaalia huko kukuungeni mkono kwa (Malaika) hizo Roho safi ila ni kuwa ni kukupeni khabari njema, kama bishara kwenu kuwa mtashinda, mpate kutua nyoyo na msonge mbele. Na Mwenyezi Mungu anakusaidieni, na wala ushindi hauji ila kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye kushinda, ambaye anaye panga mambo kwa pahala pake kwa mujibu wa ujuzi wake usio pitikiwa na chochote.
11 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 011
إِذۡ يُغَشِّيكُمُ ٱلنُّعَاسَ أَمَنَةٗ مِّنۡهُ وَيُنَزِّلُ عَلَيۡكُم مِّنَ ٱلسَّمَآءِ مَآءٗ لِّيُطَهِّرَكُم بِهِۦ وَيُذۡهِبَ عَنكُمۡ رِجۡزَ ٱلشَّيۡطَٰنِ وَلِيَرۡبِطَ عَلَىٰ قُلُوبِكُمۡ وَيُثَبِّتَ بِهِ ٱلۡأَقۡدَامَ
Alipo kufunikeni kwa usingizi uwe ni uaminisho kutoka kwake, na akakuteremshieni maji kutoka mbinguni ili kukusafisheni kwayo na kukuondoleeni uchafu wa Shet'ani, na kuzipa nguvu nyoyo zenu, na kuitia imara miguu yenu.
Enyi Waumini! Kumbukeni wakati mlipo ingiwa khofu kwa upungufu wa maji, na kuwaogopa maadui. Mwenyezi Mungu alikupeni utulivu, kwa kukuleteeni usingizi, mkalala mkatua. Akakuteremshieni maji kutoka mbinguni mkajisafishia, na mkauondoa wasiwasi wa Shetani, na nyoyo zenu zikawa imara kwa msaada wa Rahmani na pia ardhi ikashikamana kwa hayo maji, na miguu yenu ikaweza kukanyaga bila ya kudidimia katika mchanga. Aya hii inaashiria fadhila ya Mwenyezi Mungu Mtukufu juu ya wapiganaji Waumini kwa kupatikana hali ya amani kwa kupumzika kwa usingizi, na kuteremka mvua kwa kujitahirisha na kukoga, na kushikamana mchanga kwa kuwepo maji, basi nyayo zikasimama imara. Inajuulikana kuwa mchanga laini unawaletea taabu wapiganaji na unakuwa pingamizi katika kwenda huku na huko ambako ni katika dharura za vita muhimu. Na aya ya pili inaeleza maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwaambia Malaika wawathibitishe Waumini na watie khofu katika nyoyo za makafiri. Na ni maarufu kuwa khofu ikiwatawala askari katika midani huwaletea kuemewa. Na katika Aya hii tukufu panaashiriwa pahali pa kupiga napo ni juu ya shingo na kuvikata vidole vinavyo kamata silaha mkononi.
12 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 012
إِذۡ يُوحِي رَبُّكَ إِلَى ٱلۡمَلَـٰٓئِكَةِ أَنِّي مَعَكُمۡ فَثَبِّتُواْ ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْۚ سَأُلۡقِي فِي قُلُوبِ ٱلَّذِينَ كَفَرُواْ ٱلرُّعۡبَ فَٱضۡرِبُواْ فَوۡقَ ٱلۡأَعۡنَاقِ وَٱضۡرِبُواْ مِنۡهُمۡ كُلَّ بَنَانٖ
Mola wako Mlezi alipo wafunulia Malaika: Hakika Mimi ni pamoja nanyi, basi watieni nguvu walio amini. Nitatia woga katika nyoyo za walio kufuru. Basi wapigeni juu ya shingo na wapigeni kwenye kila ncha za vidole.
Enyi Waumini! Kumbukeni pale Mwenyezi Mungu alipo wafunulia wale wenye Roho zilio t'ahirika, yaani Malaika, watie ndani ya nyoyo zenu kuwa Mimi ni pamoja nanyi, nakuungeni mkono, na ninakusaidieni, kwa kuwaambia: Zitieni nguvu nyoyo za walio amini, wait'ii Haki na wapigane katika Njia ya Mwenyezi Mungu. Na Mimi nitaifanya khofu izitawale nyoyo za washirikina, nao watakuogopeni. Nanyi enyi Waumini! Wapigeni vichwani mwao vilio juu ya shingo zao, na kateni vidole vyao vinavyo kamata panga.
13 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 013
ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمۡ شَآقُّواْ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥۚ وَمَن يُشَاقِقِ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥ فَإِنَّ ٱللَّهَ شَدِيدُ ٱلۡعِقَابِ
Hayo ni kwa sababu wamemuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake basi Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
Ukawa ushindi na kuungwa mkono nyinyi, na kwao ni kitisho na fazaa, kwani wao walikuwa upande mmoja, na Mwenyezi Mungu na Mtume wake walikuwa upande mwengine, kwa kuwa wao walimpinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Basi ndio Mwenyezi Mungu anawateremshia adhabu chungu. Na adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali.
14 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 014
ذَٰلِكُمۡ فَذُوقُوهُ وَأَنَّ لِلۡكَٰفِرِينَ عَذَابَ ٱلنَّارِ
Ndio hivyo! Basi ionjeni! Na bila ya shaka makafiri wana adhabu ya Moto.
Enyi Waumini! Hivyo ndio vita, basi vionjeni, na muwe na yakini kuwa mtapata nusura na kuungwa mkono. Na wanao pinga Ishara za Mwenyezi Mungu watapata adhabu nyengine Siku ya Kiyama, nayo ni adhabu ya Moto.
15 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 015
يَـٰٓأَيُّهَا ٱلَّذِينَ ءَامَنُوٓاْ إِذَا لَقِيتُمُ ٱلَّذِينَ كَفَرُواْ زَحۡفٗا فَلَا تُوَلُّوهُمُ ٱلۡأَدۡبَارَ
Enyi Mlio amini! Mkikutana na walio kufuru vitani msiwageuzie mgongo.
Enyi mlio isadiki Haki na mkait'ii! Mkikutana na wale walio kufuru katika uwanja wa vita nao wanakujieni kwa wingi wao, msiwakimbie mkazipa mgongo panga zao.
16 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 016
وَمَن يُوَلِّهِمۡ يَوۡمَئِذٖ دُبُرَهُۥٓ إِلَّا مُتَحَرِّفٗا لِّقِتَالٍ أَوۡ مُتَحَيِّزًا إِلَىٰ فِئَةٖ فَقَدۡ بَآءَ بِغَضَبٖ مِّنَ ٱللَّهِ وَمَأۡوَىٰهُ جَهَنَّمُۖ وَبِئۡسَ ٱلۡمَصِيرُ
Na atakaye wageuzia mgongo wake siku hiyo - isipo kuwa kwa mbinu za vita au kuungana na kikosi - basi atakuwa amestahiki ghadhabu ya Mwenyezi Mungu. Na pahala pake ni Jahannamu, na huo ni mwisho muovu.
Na asiye wakaabili uso kwa uso, basi Mwenyezi Mungu amekasirika naye, na marejeo yake ni Motoni. Na huo ndio mwisho muovu kweli. Na mwenye kuacha kuwakaabili kwa kuwa ni hila na mbinu za vita, au kaacha kikosi kwenda jiunga na kikosi kingine cha Waumini apate kuwa na nguvu zaidi za mpambano, huyo hana dhambi.
17 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 017
فَلَمۡ تَقۡتُلُوهُمۡ وَلَٰكِنَّ ٱللَّهَ قَتَلَهُمۡۚ وَمَا رَمَيۡتَ إِذۡ رَمَيۡتَ وَلَٰكِنَّ ٱللَّهَ رَمَىٰ وَلِيُبۡلِيَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ مِنۡهُ بَلَآءً حَسَنًاۚ إِنَّ ٱللَّهَ سَمِيعٌ عَلِيمٞ
Hamkuwauwa nyinyi lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye wauwa. Na wewe hukutupa, walakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye tupa, ili awajaribu Waumini majaribio mema yatokayo kwake. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Msikizi na Mjuzi.
Na nyinyi Waumini, pale mnapo washinda, na mkawauwa mlio wauwa katika wao, basi hakika si nyinyi mlio wauwa kwa nguvu zenu, lakini ni Mwenyezi Mungu Mtukufu ndiye aliye kupeni ushindi na kuweza kuwauwa, kwa msaada wake kwenu na kutia khofu katika nyoyo zao. Na wewe Mtume, pale ulipo warushia mchanga na kokoto nyusoni mwao kuwafazaisha, si wewe ulio rusha, lakini ni Mwenyezi Mungu Mtukufu ndiye aliye rusha, na wao wakafazaika. Na hayo Mwenyezi Mungu ameyafanya kuwaneemesha Waumini kwa neema njema. Katika hayo pana majaribio ya nguvu kwao, ili ionekane ikhlasi yao, na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua mambo yao, Mwenye kusikia maneno yao, na Mwenye kujua mambo ya maadui zao na kauli zao pia.
18 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 018
ذَٰلِكُمۡ وَأَنَّ ٱللَّهَ مُوهِنُ كَيۡدِ ٱلۡكَٰفِرِينَ
Ndio hivyo! Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kudhoofisha vitimbi vya makafiri.
Huo ndio ushindi mkubwa, na Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mwenye kudhoofisha kila hila za makafiri.
19 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 019
إِن تَسۡتَفۡتِحُواْ فَقَدۡ جَآءَكُمُ ٱلۡفَتۡحُۖ وَإِن تَنتَهُواْ فَهُوَ خَيۡرٞ لَّكُمۡۖ وَإِن تَعُودُواْ نَعُدۡ وَلَن تُغۡنِيَ عَنكُمۡ فِئَتُكُمۡ شَيۡـٔٗا وَلَوۡ كَثُرَتۡ وَأَنَّ ٱللَّهَ مَعَ ٱلۡمُؤۡمِنِينَ
Kama mnataka hukumu basi hukumu imekwisha kujieni. Na mkiacha itakuwa ndio kheri kwenu. Na mkirejea Sisi pia tutarejea. Na jeshi lenu halitakufaeni kitu, japo likiwa kubwa. Kwani hakika Mwenyezi yu pamoja na Waumini.
Ikiwa nyinyi washirikina mlikuwa mkining'inia mapazia ya Al Kaaba na huku mnaomba yapambanuliwe baina yenu na Waumini ijuulikane haki ipo wapi, basi sasa imekwisha kujieni hukumu ya kupambanua, na ushindi si wenu, bali ni wa Waumini. Na nyinyi mkirejea tena kufanya uadui Nasi tutakushindeni tena. Wala kukusanyika kwenu kwa ajili ya madhambi hakutakufaeni kitu! Hata ikiwa idadi yenu kubwa vipi! Kwani hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na wanao isaidiki Haki na wanaikubali.
20 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 020
يَـٰٓأَيُّهَا ٱلَّذِينَ ءَامَنُوٓاْ أَطِيعُواْ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥ وَلَا تَوَلَّوۡاْ عَنۡهُ وَأَنتُمۡ تَسۡمَعُونَ
Enyi mlio amini! Mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msijiepushe naye, nanyi mnasikia.
Enyi mlio isadiki Haki, na mkaifuata! Hakika mmejua ushindi umepatikana kwa msaada wa Mwenyezi Mungu na kumt'ii Mtume wake. Basi endeleeni kumt'ii Mwenyezi Mungu na Mtume. Wala msiupuuze wito wa Mtume anao itia Haki, nanyi mnamsikia na mnafahamu ayasemayo.
21 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 021
وَلَا تَكُونُواْ كَٱلَّذِينَ قَالُواْ سَمِعۡنَا وَهُمۡ لَا يَسۡمَعُونَ
Wala msiwe kama wale wanao sema: Tumesikia, na kumbe hawasikii.
Wala msiwe kama wanaafiki wanao sema: Tumeisikia Haki na tumefahamu. Lakini hawaifuati wala hawaiamini. Basi wamekuwa kama wasio sikia.
22 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 022
۞إِنَّ شَرَّ ٱلدَّوَآبِّ عِندَ ٱللَّهِ ٱلصُّمُّ ٱلۡبُكۡمُ ٱلَّذِينَ لَا يَعۡقِلُونَ
Hakika vinyama viovu mbele ya Mwenyezi Mungu ni vile viziwi na bubu visio tumia akili zao.
Hao washirikina na wanaafiki ni kama wanyama waovu kabisa walio sibiwa na uziwi, kwa hivyo hawasikii; na wakasibiwa na ububu, kwa hivyo hawasemi. Basi wao ni viziwi kwa Haki, na hivyo hawasikii, wala hawaitamki na hawaielewi!!
23 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 023
وَلَوۡ عَلِمَ ٱللَّهُ فِيهِمۡ خَيۡرٗا لَّأَسۡمَعَهُمۡۖ وَلَوۡ أَسۡمَعَهُمۡ لَتَوَلَّواْ وَّهُم مُّعۡرِضُونَ
Na Mwenyezi Mungu angeli jua wema wowote kwao ange wasikilizisha, na lau ange wasikilizisha wangeli geuka wakapuuza.
Na Mwenyezi Mungu kwa ilimu yake ya tangu na tangu lau angeli ona ndani yao kuwa, katika hali yao hivi sasa, itakuja patikana kheri yoyote kwao hao kwa nafsi zao, na kwa watu, na kwa Haki, basi angeli wafanya wasikie kusikia kwa kuongoka hata Haki ikaingia akilini mwao. Na hata wangeli isikia na wakaifahamu Haki basi bado wasingeli ifuata. Na mapuuza hayawaachi kwa kuzidiwa na pumbao.
24 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 024
يَـٰٓأَيُّهَا ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ ٱسۡتَجِيبُواْ لِلَّهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُمۡ لِمَا يُحۡيِيكُمۡۖ وَٱعۡلَمُوٓاْ أَنَّ ٱللَّهَ يَحُولُ بَيۡنَ ٱلۡمَرۡءِ وَقَلۡبِهِۦ وَأَنَّهُۥٓ إِلَيۡهِ تُحۡشَرُونَ
Enyi mlio amini! Muitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapo kuitieni jambo la kukupeni uzima wa milele. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba hakika kwake Yeye tu mtakusanywa.
Enyi mlio isadiki Haki na mkaifuata! Muitikieni Mwenyezi Mungu kwa kufikisha anayo kuamrisheni. Na muitikieni Mtume katika vile anavyo fikisha anayo yaamrisha Mwenyezi Mungu, pale anapo kuiteni Mtume kufuata amri za Mwenyezi Mungu ambazo zitakuleteeni uzima wa miili yenu, na roho zenu, na akili zenu, na nyoyo zenu. Na mjue kwa yakini kuwa Mwenyezi Mungu ni Mwenya kuangalia nyoyo zenu. Huzielekeza atakavyo. Basi Yeye huingilia baina yenu na nyoyo zenu zinapo ingiliwa na matamanio, Yeye basi hukuokoeni nayo ikiwa nyinyi wenyewe mnajielekeza kwenye Njia iliyo nyooka. Na nyinyi nyote mtakusanywa kwake Siku ya Kiyama, na huko ndiko malipo yatakuwa.
25 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 025
وَٱتَّقُواْ فِتۡنَةٗ لَّا تُصِيبَنَّ ٱلَّذِينَ ظَلَمُواْ مِنكُمۡ خَآصَّةٗۖ وَٱعۡلَمُوٓاْ أَنَّ ٱللَّهَ شَدِيدُ ٱلۡعِقَابِ
Na jikingeni na Fitna ambayo haitowasibu walio dhulumu peke yao kati yenu. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
Na jikingeni na Dhambi kubwa ya kufisidi jamii yenu, kama vile kuacha kwenda kwenye Jihadi, na kufarikiana mkagawana mapande mapande, na kama kuacha kuamrisha mema na kukataza maovu. Kwani Fitna hiyo, Dhambi hiyo, haiwapati wale walio dhulumu peke yao, bali inawapata wote. Na mjue kuwa bila ya shaka kuwa adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali hapa duniani na Akhera pia.
26 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 026
وَٱذۡكُرُوٓاْ إِذۡ أَنتُمۡ قَلِيلٞ مُّسۡتَضۡعَفُونَ فِي ٱلۡأَرۡضِ تَخَافُونَ أَن يَتَخَطَّفَكُمُ ٱلنَّاسُ فَـَٔاوَىٰكُمۡ وَأَيَّدَكُم بِنَصۡرِهِۦ وَرَزَقَكُم مِّنَ ٱلطَّيِّبَٰتِ لَعَلَّكُمۡ تَشۡكُرُونَ
Na kumbukeni mlipo kuwa wachache, mkionekana wanyonge katika nchi, mnaogopa watu wasikunyakueni, naye akakupeni pahala pazuri pa kukaa, na akakutieni nguvu kwa nusura yake, na akakupeni riziki nzuri ili mpate kushukuru.
Na hebu kumbukeni, enyi Waumini, katika hali ya kuwa mna nguvu, pale mlipo kuwa wachache na wanyonge. Maadui walikudhilini kwa unyonge wenu, nanyi mlishikwa na khofu wasije maadui zenu kukunyakueni. Basi tena mkahama kwa amri ya Mwenyezi Mungu, na makaazi yenu yakawa Yathrib (Madina). Na mkapata manusura kwa msaada wa Mwenyezi Mungu na tawfiki yake, na akakuruzukuni ngawira njema kutaraji mtashukuru kwa neema hii, na muendelee katika Njia ya Jihadi kulinyanyua Neno la Haki.
27 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 027
يَـٰٓأَيُّهَا ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ لَا تَخُونُواْ ٱللَّهَ وَٱلرَّسُولَ وَتَخُونُوٓاْ أَمَٰنَٰتِكُمۡ وَأَنتُمۡ تَعۡلَمُونَ
Enyi mlio amini! Msimfanyie khiana Mwenyezi Mungu na Mtume, wala msikhini amana zenu, nanyi mnajua.
Enyi mlio isadiki Haki mkaifuata! Haikufaliini kumkhini Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwa kufanya urafiki na maadui wa Haki, na kukhuni katika ngawira, au kwa kuacha kwenda kwenye Jihadi. Wala msikhuni amana mnazo pewa nanyi mnajua amri na makatazo yake.
28 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 028
وَٱعۡلَمُوٓاْ أَنَّمَآ أَمۡوَٰلُكُمۡ وَأَوۡلَٰدُكُمۡ فِتۡنَةٞ وَأَنَّ ٱللَّهَ عِندَهُۥٓ أَجۡرٌ عَظِيمٞ
Na jueni ya kwamba mali zenu na wana wenu ni Fitna (mtihani), na kwamba kwa Mwenyezi Mungu upo ujira mkubwa.
Enyi Waumini, wenye kusadiki! Jueni kuwa fitna ya nafsi zenu inatokana na kupita mpaka katika mapenzi yenu kwa watoto wenu na mali yenu. Basi isiwe kupenda kwenu kuyapenda mali na wenenu yakazidi kuliko mapenzi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu. Hayo yatakuharibieni mambo yenu. Na jueni kuwa malipo ya Mwenyezi Mungu yanakutosheni kuliko mali na watoto.
29 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 029
يَـٰٓأَيُّهَا ٱلَّذِينَ ءَامَنُوٓاْ إِن تَتَّقُواْ ٱللَّهَ يَجۡعَل لَّكُمۡ فُرۡقَانٗا وَيُكَفِّرۡ عَنكُمۡ سَيِّـَٔاتِكُمۡ وَيَغۡفِرۡ لَكُمۡۗ وَٱللَّهُ ذُو ٱلۡفَضۡلِ ٱلۡعَظِيمِ
Enyi mlio amini! Mkimcha Mwenyezi Mungu atakupeni kipambanuo, na atakufutieni makosa, na atakusameheni, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kubwa.
Enyi mlio isadiki Haki na mkaifuata! Mkizinyenyekea amri za Mwenyezi Mungu kwa siri na dhaahiri, Mwenyezi Mungu atakujaalieni katika nafsi zenu uwezo wa kupambanua baina ya Haki na upotovu, na atakutunukieni ushindi wa kutenga baina yenu na maadui zenu, na atakusitirieni maovu yenu yaondoke, naye akusameheni. Na Yeye Subhanahu daima ni Mwenye fadhila kubwa.
30 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 030
وَإِذۡ يَمۡكُرُ بِكَ ٱلَّذِينَ كَفَرُواْ لِيُثۡبِتُوكَ أَوۡ يَقۡتُلُوكَ أَوۡ يُخۡرِجُوكَۚ وَيَمۡكُرُونَ وَيَمۡكُرُ ٱللَّهُۖ وَٱللَّهُ خَيۡرُ ٱلۡمَٰكِرِينَ
Na walipo kupangia mpango walio kufuru wakufunge, au wakuuwe, au wakutoe. Wakapanga mipango yao, na Mwenyezi Mungu akapanga yake. Na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa mipango.
Na kumbuka ewe Nabii, neema za Mwenyezi Mungu zilio juu yako, pale washirikina walipo panga njama kukutia nguvuni - ama wakufunge, au wakuuwe, au wakutoe mji! Hakika walikupangia mipango miovu! Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alikupangia utokane na shari yao. Na mpango wa Mwenyezi Mungu ndio wa kheri, na una nguvu zaidi, na ndio wenye kushinda.
31 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 031
وَإِذَا تُتۡلَىٰ عَلَيۡهِمۡ ءَايَٰتُنَا قَالُواْ قَدۡ سَمِعۡنَا لَوۡ نَشَآءُ لَقُلۡنَا مِثۡلَ هَٰذَآ إِنۡ هَٰذَآ إِلَّآ أَسَٰطِيرُ ٱلۡأَوَّلِينَ
Na wanapo somewa Aya zetu, wao husema: Tumesikia. Na lau tungeli penda tunge sema kama haya. Haya si chochote ila hadithi za watu wa kale tu.
Na ewe Nabii! Kumbuka inda ya washirikina ulipo kuwa ukiwasomea Aya za Qur'ani Tukufu, nazo ni Ishara zetu. Ujahili wao na ghururi yao iliyo pita kiasi iliwapelekea kusema: Tungeli taka kusema kama isemavyo hii Qur'ani tungeli sema; kwani humu hamna chochote ila visa walivyo viandika watu wa kale!
32 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 032
وَإِذۡ قَالُواْ ٱللَّهُمَّ إِن كَانَ هَٰذَا هُوَ ٱلۡحَقَّ مِنۡ عِندِكَ فَأَمۡطِرۡ عَلَيۡنَا حِجَارَةٗ مِّنَ ٱلسَّمَآءِ أَوِ ٱئۡتِنَا بِعَذَابٍ أَلِيمٖ
Na walipo sema: Ee Mwenyezi Mungu! Ikiwa haya ni kweli itokayo kwako basi tunyeshee mawe kutoka mbinguni, au tuletee adhabu yoyote iliyo chungu.
Na kumbuka, ewe Nabii, vipi walivyo kuwa wanakupinga na kumpinga Mwenyezi Mungu hata kwa inda yao wakasema kumwambia Mwenyezi Mungu, Mola wao Mlezi: Ikiwa haya unayo kuja nayo ni mambo madhbuti, basi zijaalie mbingu zitunyeshee mawe, au tuletee adhabu yoyote iliyo kali yenye uchungu!
33 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 033
وَمَا كَانَ ٱللَّهُ لِيُعَذِّبَهُمۡ وَأَنتَ فِيهِمۡۚ وَمَا كَانَ ٱللَّهُ مُعَذِّبَهُمۡ وَهُمۡ يَسۡتَغۡفِرُونَ
Na Mwenyezi Mungu hakuwa wa kuwaadhibu nawe umo pamoja nao, wala Mwenyezi Mungu si wa kuwaadhibu na hali ya kuwa wanaomba msamaha.
Si katika hikima ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwaadhibu katika dunia kwa adhabu kali na hali wewe upo miongoni mwao unaitia Haki, nawe unataraji asaa wataitikia. Wala si mtindo wa Mwenyezi Mungu kuwaadhibu wenye kuasi nao wangali wanamuomba maghfira na wamo kuyavua yale waliyo nayo.
34 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 034
وَمَا لَهُمۡ أَلَّا يُعَذِّبَهُمُ ٱللَّهُ وَهُمۡ يَصُدُّونَ عَنِ ٱلۡمَسۡجِدِ ٱلۡحَرَامِ وَمَا كَانُوٓاْ أَوۡلِيَآءَهُۥٓۚ إِنۡ أَوۡلِيَآؤُهُۥٓ إِلَّا ٱلۡمُتَّقُونَ وَلَٰكِنَّ أَكۡثَرَهُمۡ لَا يَعۡلَمُونَ
Lakini wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu, na hali ya kuwa wanawazuilia watu Msikiti Mtakatifu? Wala wao hawakuwa ndio walinzi wake, bali walinzi wake hawakuwa ila wacha-Mngu tu. Lakini wengi katika wao hawajui.
Hakika hali yao iliyo sasa inaruhusu kuwaadhibu, kwani wanawazuia watu wasiutumie Msikiti ambao Mwenyezi Mungu ameutukuza kwa kuharimisha vita karibu yake. Lakini Mwenyezi Mungu anawaakhirisha kwa alivyo wakadiria katika ujuzi wake kuwa wengi wao watakuja amini. Wao wakati huu wa sasa sio walinzi wa kuunusuru huo Msikiti Mtukufu, bali wao wameunajisi kwa kutia ibada ya masanamu ndani yake. Ama wa kuunusuru hakika ni Waumini, wenye kumt'ii Mwenyezi Mungu. Lakini wengi katika washirikina hawaijui Dini, wala hawajui cheo cha Nyumba hiyo Tukufu.
35 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 035
وَمَا كَانَ صَلَاتُهُمۡ عِندَ ٱلۡبَيۡتِ إِلَّا مُكَآءٗ وَتَصۡدِيَةٗۚ فَذُوقُواْ ٱلۡعَذَابَ بِمَا كُنتُمۡ تَكۡفُرُونَ
Na haikuwa ibada yao kwenye hiyo Nyumba (Al Kaaba) ila ni kupiga miunzi na makofi. Basi onjeni adhabu kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru.
Na maombi yao kwenye Nyumba hii Tukufu (Al Kaaba) si chochote ila ni kupiga myunzi na makofi. Ilivyo kuwa hiyo ndiyo hali yenu, basi wacha mauti yakupateni, na yaonjeni katika uwanja wa vita, upate kubaidika (kuwa mbali) ushirikina kutokana na Al Kaaba. Na kuuliwa huko kwenu ni kwa sababu ya ukafiri wenu.
36 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 036
إِنَّ ٱلَّذِينَ كَفَرُواْ يُنفِقُونَ أَمۡوَٰلَهُمۡ لِيَصُدُّواْ عَن سَبِيلِ ٱللَّهِۚ فَسَيُنفِقُونَهَا ثُمَّ تَكُونُ عَلَيۡهِمۡ حَسۡرَةٗ ثُمَّ يُغۡلَبُونَۗ وَٱلَّذِينَ كَفَرُوٓاْ إِلَىٰ جَهَنَّمَ يُحۡشَرُونَ
Hakika wale walio kufuru hutoa mali yao ili kuzuilia Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watayatoa, kisha yatakuwa juu yao majuto, na kisha watashindwa. Na wale walio kufuru watakusanywa kwenye Jahannam.
Hakika hao wanao zipinga Ishara za Mwenyezi Mungu na wanamshirikisha na miungu mingine, hutoa mali yao ili wawazuie watu wasiifuate Imani ya Haki! Nao wataendelea kutoa hayo mali, kisha hayo mali, kwa kuwapotea bure bila ya pato walitakalo, yatawaletea majuto na machungu. Na katika uwanja wa mpambano watashindwa hapa duniani, na kisha watakusanywa wote katika Jahannam, wakibaki na ukafiri wao.
37 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 037
لِيَمِيزَ ٱللَّهُ ٱلۡخَبِيثَ مِنَ ٱلطَّيِّبِ وَيَجۡعَلَ ٱلۡخَبِيثَ بَعۡضَهُۥ عَلَىٰ بَعۡضٖ فَيَرۡكُمَهُۥ جَمِيعٗا فَيَجۡعَلَهُۥ فِي جَهَنَّمَۚ أُوْلَـٰٓئِكَ هُمُ ٱلۡخَٰسِرُونَ
Ili Mwenyezi Mungu apate kuwa pambanua walio waovu na walio wema, na kuwaweka waovu juu ya waovu wengine, na kuwarundika wote pamoja, na kuwatupa katika Jahannam. Hao ndio walio khasirika.
Kwa kushindwa makafiri duniani na kuadhibiwa Motoni Akhera Mwenyezi Mungu anapambanua aliye khabithi wa roho na vitendo na maneno, awe mbali na aliye mwema wa roho yake na moyo wake. Na awafanye wale waovu makhabithi wapandane wenyewe kwa wenyewe, huyu juu ya huyu, na awatie Motoni Siku ya Kiyama. Na hao washirikina mafisadi ndio wenye kukhasiri peke yao, duniani na Akhera.
38 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 038
قُل لِّلَّذِينَ كَفَرُوٓاْ إِن يَنتَهُواْ يُغۡفَرۡ لَهُم مَّا قَدۡ سَلَفَ وَإِن يَعُودُواْ فَقَدۡ مَضَتۡ سُنَّتُ ٱلۡأَوَّلِينَ
Waambie wale walio kufuru: Wakikoma watasamehewa yaliyo kwisha pita. Na wakiyarudia basi imekwisha pita mifano ya wa zamani.
Hakika juu ya vitisho hivi, mlango wa matarajio ungali wazi. Basi ewe Nabii wa rehema! Waambie hawa wapinzani kuwa wakikoma, wakaacha inadi yao na ushirikina wao, basi hapana shaka Mwenyezi Mungu atawasamehe vile vitendo vyao vilivyo kwisha pita. Na wakiendelea na upotovu wao, na wakarudia tena kukupigeni vita, basi mwendo wa Haki kwa walio tangulia umethibiti utakuwa ule ule, nao ni kuwa Haki lazima iushinde upotovu, pindi ikiwa wale watu wa Haki wakishika ut'iifu na njia za ushindi.
39 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 039
وَقَٰتِلُوهُمۡ حَتَّىٰ لَا تَكُونَ فِتۡنَةٞ وَيَكُونَ ٱلدِّينُ كُلُّهُۥ لِلَّهِۚ فَإِنِ ٱنتَهَوۡاْ فَإِنَّ ٱللَّهَ بِمَا يَعۡمَلُونَ بَصِيرٞ
Na piganeni nao mpaka isiwepo fitna na mateso, na Dini yote iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Lakini wakiacha, basi hakika Mwenyezi Mungu anayaona wanayo yatenda.
Na endeleeni kuwapiga vita washirikina mpaka waache kuharibu itikadi za Waumini kwa kuwatesa na kuwaudhi. Wakiacha ukafiri na kuwaudhi Waumini, na wakamsafia Dini Mwenyezi Mungu, basi Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuvijua vitendo vyao, na atawalipa kwavyo.
40 - Al-Anfal (The Spoils of War) - 040